• HABARI MPYA

    Thursday, September 20, 2012

    MANJI AWAKA 3-0 ZA MTIBWA, TIMU KUFIKIA KITI MOTO DAR

    Viongozi wa Yanga, kushoto Mussa Katabaro na Seif Ahmad 'Magari' wakiwa taaban Uwanja wa Jamhuri jana

    Na Mahmoud Zubeiry, Morogoro
    KIPIGO cha mabao 3-0 ambacho Yanga imechapwa na wenyeji Mtibwa Sugar ya Turiani, Morogoro kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini hapa jana, katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kimemkasirisha Mwenyekiti wa klabu hiyo, Yussuf Mehboob Manji amefoka mno.
    Chanzo chetu cha habari kutoka Yanga leo, kimesema kwamba Manji alipiga simu kuulizia matokeo na kufoka sana baada ya kuambiwa timu imefungwa mabao 3-0. “Manji amekasirika sana, alipiga simu, alipoambiwa timu imefungwa akafoka sana,”kilisema chanzo chetu kutoka Yanga jana.
    Viongozi wa Yanga walioambatana na timu hapa mjini hapa, akiwemo Seif Ahmad ‘Magari’ na Mussa Katabaro walisikitishwa na hali hiyo na hawakuwa tayari kusema chochote.
    Manji akizungumza na wachezaji baada ya kutwaa Kombe la Kagame. 
    Lakini habari za ndani zinasema hali hiyo imeanza kuwashangaza hata makocha na wachezaji, kwa sababu timu yao ilikuwa vizuri na ghafla inaanza kubadilika.
    Yanga itarejea Dar es Salaam leo kuanza maandalizi ya mchezo wao ujao, dhidi ya JKT Ruvu Jumamosi, lakini kabla ya hapo kutakuwa na kikao kikali juu ya mwenedo wa timu katika mechi mbili za mwanzo.
    Katika mchezo wa kwanza ambao Yanga ililazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons mjini Mbeya, kocha Mbelgiji wa klabu hiyo alilalamikia malazi mabovu katika hoteli waliyofikishiwa, lakini jana alisema malazi yalikuwa mazuri na wachezaji walikuwa vizuri kabla ya mechi.
    Labda ni Uwanja mbovu, hiyo ni sababu iliyobakia, lakini mechi ijayo Yanga itacheza kwenye Uwanja mzuri wa Taifa, Dar es Salaam waliouzoea dhidi ya JKT ambayo jana ilipigwa 2-0 na Simba pungufu.
    Mambo mawili yanatazamwa kwa sasa, moja mfumo wa kucheza kwa kujihami zaidi na pili kujiamini kupita kiasi, labda yanaweza kuwa yanachangia matokeo mabaya. Wachezaji wa Yanga kwa sasa wanaonekana ‘kujisikia’ mno baada ya matokeo mazuri ya awali, ikiwemo kutwaa Kombe la Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame na hawachezi kwa kujituma kama mwanzo.
    Kuhusu mfumo, hakuna kilichobadilika sana Yanga, bado ni ule ule wa kutumia mabeki watupu wingi ya kushoto, ambao uliwapa Kombe la Kagame, labda tatizo la ‘kujisikia’ kwa wachezaji na kudharau timu pinzani linaweza kuwa la msingi katika suala hili.  
    Katika mchezo wa jana, Yanga ilizidiwa mno na hadi mapumziko, tayari Mtibwa Sugar walikuwa mbele kwa mabao 2-0, yaliyotiwa kimiani na beki wa kati, Dickson Daudi dakika ya 11 akiunganisha kwa kichwa kona ya beki wa kushoto Malika Ndeule.
    Bao hilo lilitokana na uzembe wa mabeki wa Yanga ambao walishindwa kumuweka ulinzi mchezaji mrefu kuliko wote, Daudi.
    Yanga walijaribu kutaka kusawazisha, lakini mipango yao haikuwa na tija na kujikuta wakiendelea kushambuliwa na dakika ya 43, Hussein Javu aliwainua tena vitini mashabiki wa Simba waliokuwa wakiwashangilia kwa nguvu leo kwa kufunga bao la pili.
    Kwa ujumla kipindi cha kwanza, Yanga walicheza ovyo- pasi zao nyingi zilikuwa hazifiki, walishindwa kuwabana wapinzani wao na zaidi Haruna Niyonzima alishindwa kuiongoza vema timu, jambo ambalo lilifamnya kiungo mkabaji Athumani Iddi ‘Chuji’ kupanda mbele zaidi kusaidia, ingawa haikusaidia.
    Mabeki wawili wa kati wa Mtibwa, Daudi na Salvatory Ntebe waliwadhibiti vema washambuliaji wawili wa Yanga, Hamisi Kiiza na Saidi Bahamnuzi katika dakika 45 za kipindi cha kwanza.
    Kipindi cha pili, Kocha wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintfiet alianza kwa mabadiliko akiwatoa Frank Damayo na David Luhende na kuwaingiza Simon Msuva na Stefano na Mwasyika, lakini bado ukuta wa Mtibwa ulikuwa mgumu mbele ya Watoto wa Jangwani.
    Katika kuongeza mashambulizi, Mtakatifu Tom alimtoa beki Mbuyu Twite na kumuingiza na mshambuliaji Didier Kavumbangu, lakini bado mambo yaliendelea kuwa magumu kwa Yanga.
    Dakika ya 86 Hussein Javu aliifungia Mtibwa bao la tatu kwa shuti la mbali, wakitoka kushambuliwa na kufikia hapo, Yanga ‘walikufa’ na mashabiki wao wakaanza kuuacha Uwanja wa Jamhuri.
    Huu unakuwa mchezo wa pili kwa Yanga tangu kuanza kwa ligi wakiwasononesha mashabiki wao, baada ya mechi ya kwanza kulazimishwa sare ya bila kufungana na Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.   
    Waswahili wanasema siku ya kufa nyani, miti yote huteleza, Hamisi Kiiza alipaisha mkwaju wa penalti dakika ya 89, baada ya Daudi kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
    Yanga SC; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, , Mbuyu Twite/Kavumbangu, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan, Athumani Iddi ‘Chuji’, Frank Domayo/Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Said Bahanuzi, Hamisi Kiiza na David Luhende/Stefano Mwasyika.
    Mtibwa Sugar; Shaaban Hassan Kado, Malika Ndeule, Issa R Issa, Dickson Daudi, Salvatory Ntebe, Shaaban Nditi, Jamal Mnyate/Babu Ally Seif, Awadh Juma, Hussein Javu, Shaaban Kisiga ‘Malone’ na Vincent Barnabas/Ally Mohamed ‘Gaucho’.
    Katika mechi nyingine,  Simba SC imeendeleza wimbi la ushindi, baada ya kuichapa JKT Ruvu mabao 2-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, licha ya kucheza pungufu baada ya Emanuel Okwi kutolewa nje kwa kadi nyekundu.
    Mabao ya Simba yalitiwa kimiani na viungo Amri Kiemba na Haruna Moshi ‘Boban’ na kwa matokeo hayo, Simba inaendelea kuongoza ligi kwa kufikisha pointi sita, baada ya awali kuifunga African Lyon 3-0. 
    Simba SC; Juma Kaseja, Nassor Masoud ‘Chollo’, Amir Maftah, Shomary Kapombe, Juma Nyosso, Mwinyi Kazimoto, Amri Kiemba, Haruna Moshi ‘Boban’, Daniel Akuffo, Mrisho Ngassa na Emanuel Okwi.
    Katika mechi nyingine za ligi hiyo, Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza Azam imelazimishwa sare ya 2-2 na wenyeji Toto African, Uwanja wa Kaitaba Bukoba, wenyeji Kagera Sugar wametoka sare ya bila kufunga na JKT Oljoro ya Arusha, wakati Uwanja wa Sokoine Mbeya, wenyeji Prisons wametoka sare ya 1-1 na Coastal Union ya Tanga na kwenye Uwanja wa Chamazi, African Lyon imeifunga Polisi Morogoro 1-0, wakati Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Ruvu Shooting imeifunga 2-1 Mgambo JKT.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MANJI AWAKA 3-0 ZA MTIBWA, TIMU KUFIKIA KITI MOTO DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top